Jumatano, 29 Machi 2017

Dkt. JOHANSEIN RUTAIHWA: KIATU CHA UBUNGE WA AFRIKA MASHARIKI KINANITOSHA, NIVALISHENI NIWATUMIKIE



Nafasi ya ubunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ni sehemu mojawapo ambayo nchi inapata wawakilishi wake katika Jumuiya hiyo ukiachana  na nafasi ya ajira za moja kwa moja zitolewazo na Jumuiya hii. Ni sehemu nyeti sana kwa nchi katika kupata watetezi kwenye masuala yanayohusu nchi kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki. Hawa ni wawakilishi wetu hatupaswi kufany makosa kwenye teuzi zao, tunapaswa  tuchague watu makini wenye uwezo wa kuliwakilisha vyema taifa letu. Hatutakiwi kuruhusu nchi yetu imezwe na nchi nyingine wanachama wa Jumuiya hiyo ya Afrika Mashariki. Mchango na umuhimu wa Tanzania kwenye nchi za Afrika Mashariki, kati na Afrika kwa ujumla wake lazima ubaki pale pale kama ilivyokuwa enzi za Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere. Tunataka Tanzania iwe kigezo kwenye nyanja zote kisiasa, kiuchumi, kijeshi na kijamii. Maslahi ya Taifa kimataifa yanategemea zaidi uwezo wetu wa kushawishi.
Kutokana na umuhimu huo kwa taifa, tunahitaji wawakilishi wanaojiweza katika kushawishi, wanaojua historia yetu, vipaumbale vyetu lakini vilevile wanaofahamu vyema lugha ya kingereza ambayo ndiyo lugha rasmi ya mawasiliano ndani ya jumuiya hiyo. Kwahiyo tunapotafuta wawakilishi lazima tuangalie ujuzi wao kwenye kuzungumza lugha ya kiingereza na uwezo wao wa kushawishi kupitia ujenzi wa hoja madhubuti zenye uzito na mashiko.

NAONA LUGHA GONGANA KATIKA UJENZI WA MNARA WA BABERI

Nakumbuka siku za nyuma Chama cha Mapinduzi CCM kilielemewa sana na upinzani wakati wa katibu mkuu mzee wetu Yusuph Makamba na baadae Bwana Wilson Mkama. Upinzani ulishika hatamu, kila kona walitawala wao kuanzia kwenye vyombo mbalimbali vya habari, mitaani, kwenye vijiwe vya kahawa na hadi maofisini. Kila siku hoja nzito zilikuwa zikiibuliwa na upinzani, hoja za kukidhoofisha Chama na Serikali yake hasa kwenye mambo ya ufisadi.
Mabadiliko ya Sekretarieti kutoka ya Yusuph Makamba hadi ya Mheshimiwa Abdurahamani Kinana, kama katibu mkuu wa chama, Philip Mangula, kama makamu mwenyekiti huku Mheshimiwa Nape Nnauye, akiwa kama katibu Mwenezi wa Chama kulileta fikra na mawazo mapya ya kuendesha chama. Nadhani kila mtu anakumbuka kazi iliyofanywa na Sekretarieti hiyo katika kurudisha uhai wa chama. Mheshimiwa Kinana yeye kwa upande wake alizunguka nchi nzima kufufua chama na kuleta matumaini mapya kwa wanachi huku Bwana Nape Nnauye yeye kwa upande wake alikuwa shupavu na shapu kujipu hoja yoyote inayotolewa na upinzani na kuitolea ufafanuzi wa kina. Kwahakika wapinzani walimgwaya ile mbaya bwana Nape Nnauye na mara nyingi walipokuwa wakishindwa kujibu hoja zake waliishia tu kumwita mlopokaji lakini kimsingi kama katibu mwenezi aliweza kusimama katika nafasi yake vizuri na kukiweka chama katika uimara ambao umesaidia hata kukivusha vyema chama hicho katika kipindi cha uchaguzi uliyopita, uchaguzi uliokuwa na ushindani mkubwa kuwahi kutokea katika historia ya siasa za vyama vingi nchini Tanzania tangu kuasisiwa kwake mwaka 1992. Katika uchaguzi huo kama kusingelikuwa na Sekretarieti imara naamini leo hii tungelisema mambo mengine juu ya uhai wa Chama cha Mapinduzi.
Lakini leo hii asubuhi nimesikia Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amefanya mabadiliko madogo katika baraza lake la mawaziri na katika mabadiliko hayo Mheshimiwa Prof. Palamagamba Kabudi ameteuliwa kuwa Waziri wa Katiba na sheria wakati Dkt. Harrison Mwakyembe amechukua nafasi ya Mheshimiwa Nape Nnauye katika nafasi ya Uwaziri wa Habari, Michezo na Utamaduni. Ni kweli ni uamuzi wa Rais kufanya mabadiliko kadili ya matakwa yake na hakuna wa kumpangia. Na mamlaka haya amepewa kwa mujibu wa sheria na katiba ya nchi. Lakini ni muhimu kutambua mchango wa mtu katika chama na nchi. Nape Nnauye ni kijana anayehitaji kufunzwa pale anapokosea kama kijana. Kumwajibisha kama ilivyotokea sioni kama kutasaidia kuimarisha chama na kuleta mustakabari bora wa nchi. Nilidhani kama kuna kutofautiana kidogo ni muhimu zaidi kutumia vikao kumaliza tofauti hizo. Wahenga walisema Mnyonge Mnyongeni lakini haki yake mpeni. Nape Nnauye ni kijana chapakazi haswa asiyekubali kunyamaza pale anapoona kwenye mamlaka yake kuna jambo limetokea. Ni mwepesi kupaza sauti ili kutolea ufafanuzi hasa yale masuala yenye kuzua taharuki.
Kitu ninachokiona kwa sasa katika chama cha Mapinduzi chama kongwe nchini na bara la Afrika kwa ujumla wake ni kama kuna lugha gongana katika ujenzi wa mnara wa Baberi. Na nadhani matokeo ya lugha gongana katika ujenzi wa mnara ule wote tunajua kama ulivyoanishwa katika vitabu vitakatifu. Ni muhimu kama chama kinachoongoza dola kuwa makini katika maamuzi yanayochukuliwa vinginevyo tutakuja kujilaumu wenyewe kwa makosa madogo ya kimkakati tunayoyafanya. Kama mtu atajaribu kutatazama mgongoro huu kwa jicho la tatu, anaweza kubaini dhahiri kuwa kama kuna ugomvi wa kugombea fito katika ujenzi wa nyumba kitu ambacho kama haitachukuliwa hatua za haraka kutatua tatizo, huwenda ikaleta madhara makubwa kwa ustawi wa chama na nchi kwa ujumla wake. Ni muhimu kukumbuka kuwa siku zote majuto ni mjukuu. Na vita vya panzi huwa ni furaha kwa kunguru. Siku zote vyama vikongwa barani afrika hung'oka madarakani kutokana na magomvi ya wao kwa wao kama ambavyo tumeanza kushuhudia yanayotokea katika Chama cha Mapinduzi CCM.
Hivi ndivyo nianavyo mimi.

Jumamosi, 25 Machi 2017

FURSA KATIKA KILIMO CHA VIAZI LISHE, TUCHANGAMKIENI UPESI

Viazi lishe ni aina ya viazi vitamu vyenye mwonekano wa rangi ya njano kwa ndani vikimenywa. Viazi lishe ni biashara mpya katika kilimo biashara ambacho hakijamulikwa vyema na wakulima wetu. Hii ni fursa muhimu na ya kipekee kwa wakulima wanaolenga utajiri kutokana na kilimo. Kwa kifupi huku kuna pesa kuliko kawaida. Ni muhimu tukaichangamkia fursa hii. Kilimo cha viazi lishe ni kama ilivyo kwa viazi vingine vitamu ni rahisi sana ukilinganisha na aina nyingine ya kilimo.
Viazi lishe hutumia muda wa miezi mitatu toka kupandwa hadi kuvunwa. Na kama vikilimwa kwa ajili ya mbegu, vyazi hivyo hutumia miezi miwili tu na vinakuwa tayari kuvunwa na kupelekwa shambani.
Viazi lishe vina beta karotini ambayo ni chanzo muhimu cha vitamini A. Viazi lishe vinatengeneza bidhaa mbalimbali zikiwemo Chipsi, Kripsi pamoja na Unga ambao hutumika kutengenezea bidhaa mbalimbali kama vile Mikate, Keki, Maandazi, chapati, Biskuti na vitafunwa vinginevyo. Kwa kifupi, kwa kutumia viazi lishe, tunaweza kutengeza bedhaa zote ambazo unga wa ngano unatengeneza. Majani ya viazi lishe hutumika kama mboga.

Jumatano, 22 Februari 2017

TUNAUZA VIFARANGA WA AINA ZOTE KARIBUNI SANA


MAJIBU KWA MTEJA WETU BWANA UWEZO NYATIGE KUTOKA KINASORU EAST AFRICA TANZANIA LTD

BWANA UWEZO NYATIGE, ANAULIZA
"Habari za majukumu.
Nimesoma ushauri wenu juu ya ufugaji mtandaoni mbarikiwe kwa hilo.
Nimevutiwa na mradi wa utotoleshaji wa vifaranga. nina changamoto moja sijui mtanisaidiaje.
Mimi ni mkazi wa Dar es salaam wakati nyie mko Dododma.
1. Je mna watu wenye mayai hayo hapa Dar es salaam ili nikianza mradi niwe na uhakika wa mayai hayo bora ya kuku wa kienyeji walioboreshwa?
2. Je nitakapototolesha mayai hayo, vifaranga ni lazima nivilete Dodoma ili kuwauzia hao Ma Agent au mnao pia Dar wanaochukua vifaranga kwa uhakika?
Nina nia ya kujikomboa kiuchumi. naomba unisaidie hayo ili niweze kufanya maamuzi ikiwa pamoja na kujipanga kuja Dododoma kwa ajili ya Semina maalum juu ya hilo kabla sijaanza mradi.
Nashukuru kwa ushirikiano wako.
Ahsante".
MAJIBU KUTOKA KINASORU EAST AFRICA TANZANIA LTD
Bwana Uwezo Nyatige,
Awali ya yote nikushukuru kwa baraka zako kwetu lakini pili nikupongeze kwa kuwa mfuatiliaji wa mada zetu za ufugaji kupitia mitandao. Nakuhaidi kuendelea kutoa mafunzo kama hayo katika mitandao mbalimbali ya kijamii ili yaweze kuwa msaada na mwongozo kwako na kwa watu wengine pia katika uendeshaji wa miradi ya ufugaji kibiashara. Utakapoona wakati mwingine tuko kimya kwa muda isikupe hofu sisi tupo, ni kutingwa tu kidogo na majukumu ya hapa na pale lakini napenda nikuhakikishie kuwa Kinasoru East Africa Tanzania Ltd daima iko pamoja na wakulima na wafugaji kwa ujumla wake.
Naomba nianze kukujibu kwa kukuondoa shaka kuhusu umbali uliyopo baina yetu kwa maana Dodoma na DSM. Kimsingi umbali huo siyo kikwazo kitakachokufanya ushindwe kuanzisha mradi wako. Kampuni yetu inawataalamu waliyobobea katika fani hiyo na kwamba wataweza kukushauri kwa njia mbalimbali ikiwemo njia ya simu na kukutembelea huko Dar es salaam kwa mwaliko wako na baada ya kukushauri tutakupatia vitabu vya mwongozo vitakavyokusaidia kukuongoza. Vile vile Dar es saalam ni miongoni mwa mikoa iliyo na wateja wetu wengi kabisa na wote tunawashauri kwa njia ya simu na inapopatikana safari ya kuja huko tunaitumia fursa hiyo pia kuwatembelea na wateja wetu wengine. Mradi kama huo unaoutaka kuufanya tumeweza kuwaanzishia weteja wetu wengine kadhaa kuwataja japo wachache mmoja yupo Morogoro na Mwingine yuko Mwanza maeneo ya Nyasaka na wote hatchery zao zinafanyakazi vizuri sana. Ukiangalia Mwanza ni mbali kuliko Dsm lakini tumeweza kumwongoza hadi sasa na maendeleo yake ni mazuri.
Kinasoru East Africa Tanzania LTD haina vyanzo vya uhakika vya kukusanya mayai mazuri yanayofaa kwa shughuli ya utotoleshaji kwa mkoa wa Dar es salaam. Mfumo wetu wa kupata mayai ni kwa kuwatumia wafugaji tuliyowapa elimu maalum ya ufugaji wa kuku wazazi wenye kutaga mayai yanayofaa kuatamishwa na hatimae kutotolewa vifaranga. Wafugaji hawa tunawaita outgrowers. Tumewafundisha sifa za mayai yanayotakiwa kutotoleshwa yanatakiwa yaweje na namna gani yataweza kutuzwa. Pia wafugaji hao tunawafuatilia hatua kwa hautua kuona kama kweli wanazingatia mafunzo tuliyowapatia. Kwa sasa tuna outgrowers Morogoro mjini, Dakawa na Dodoma mjini. Na mtu yoyote anayehitaji mayai kutoka sehemu yoyote ya nchi yetu , tutamtumia kutoka Dodoma kwani Dodoma ndiyo kituo kikuu cha kukusanya mayai na kuyatuma kwa wateja wetu mbalimbali. Kwasababu mayai yetu yanatoka kwa wafugaji wetu mablimbali, na ili kudhibiti ubora wake kila mfugaji tumempatia namba na kwamba namba hiyo tunakuwa tumeiandika katika kila yai lililoletwa na mfugaji husika. Na ikitokea mayai hayajatotolewa na ikathibitika kuwa kutototolewa huko kwa mayai kunatokana na mayai yetu basi tunachukua jukumu la kumfidia mteja wetu, tunachofanya ni kukuuliza tu ni mayai namba ngapi au yenye alama gani ambayo hayakuweza kutotolewa ili tuweze kumtafuta mhusika wa mayai hayo. Kupitia namba hizo tutambaini mfugaji mwenye hayo mayai na hatimaye mfugaji huyo atalazimika kufidia mayai mengine kinyume cha hapo tutamwondoa katika mfumo wetu wa masoko. Wafugaji waaminifu peke yao ndiyo tunaowahitaji. Tunashukuru kupitia mfumo huu wafugaji wetu wamekuwa waelewa na waaminifu sana. Mayai wanayotuletea yamekuwa yakikidhi haja yetu. Wateja wetu wanaoagiza mayai hayo wamekuwa wakiyafurahia kwa namna yanavyototolewa vizuri lakini vilevile ule mfumo wetu wa kufidia tunaoutumia pale inapotokea mayai yameleta shida.
Utakapo totolesha mayai hayo vifaranga siyo lazima utulete Dodoma. Kazi ya Kinasoru East Africa Tanzania Ltd ni kuwaunganisha wafugaji na wateja au watotoleshaji na wateja. Tunachokifanya sisi ni kukutafutia soko la karibu yako hukohuko Dsm na ikishindikana tutakutafutia masoko katika mikoa ya jirani na mkoa wako. Lakini vilevile unapaswa kutambua kuwa Kinasoru East Africa Tanzania Ltd inakupa uhuru wewe mfugaji wa kuchagua kama ikitokea umepata soko lako la uhakika uweze kuuza bila sisi kukuingilia. Hivi ndivyo tunavyofanya kazi zetu. Siku zote lengo letu ni kumwona mkulima na mfugaji anafanya shughuli zake kibiashara ili tija ya kazi yake iweze kuonekana. Na kama kote huko itashindikana basi tutakutafutia soko Dodoma kwa wafugaji wetu na maeneo mengine ya nchi na hapa sisi tutaongeza asilimia kidogo ya gharama kutoka kwenye bei yako ili nasi tuonekana kuna shughuli tunaifanya na ndipo hapo tunapogeuka na kuwa wakala wako. Lengo letu ni kuwa hatutaki mfugaji ahangaike mwenyewe kutafuta masoko mara uzalishaji unapoanza

KUWA NA MABANDA BORA YA KUKU NI MTAJI

Unapofikiria kufanya mradi wa ufugaji wa kuku, hitajio la kwanza na la muhimu ni kuwa na mabanda bora ya kufugai kuku wako. Kwa bahati mbaya sana ujenzi wake umekuwa ghali na hivyo kuwakatisha tamaa watu wengi wanaohitaji kuanza mradi huo.
Katika hali ya kawaida vijana wengi wanaomaliza vyuo vikuu wanakuwa hawana uwezo wa kumudu kujenga mabanda hayo matokeo yake wanashindwa kufanya mradi wa ufugaji wa kuku. Laita kama kungelikuwa na watu binafsi au mashirika ya uma au serikali ikaamua kwa dhati kabisa kuwekeza katika ujenzi wa mabanda bora ya kuku halafu yakakodishwa kwa wahitaji, naamini watu wengi hususani wahitimu wa vyuo wangeweza kuyakodi mabanda hayo na kuyatumia katika biashara hii ya ufugaji wa kuku.
Mabanda ya kuku yanatakiwa yajengwe kwa kuzingatia ubora lakini vilevile na mahali husika yanapotaka kujengwa mabanda hayo ili kujua aina ya mabanda yanayofaa kujengwa kulingana hali ya hewa ya mahali hapo. Maeneo ya joto kwa mfano mikoa yote ya Pwani na Mwambao wa Bahari na Morogoro ni muhimu mabanda yake yakajengwa kwa kuweka madirisha mapana yenye kuruhusu hewa ya kutosha kuingia ndani ya mabanda hayo. Na kwa maeneo ya baridi kwa mfano mikoa ya Mbeya, Njombe, Iringa, Moshi na Arusha madirisha yake yanatakiwa yapandishwe juu sana ili kuruhusu hewa kuingia vyema lakini wakati huo huo kuku waweze kukingwa na hali ya baridi. Lakini kwa maeneo yenye joto kali na upepo wakati wa mchana na baridi wakati wa usiku kwa mfano kwa maeneo ya mikoa ya Dodoma, Singida na Tabora mabanda yake yanatakiwa yainuliwe kozi sita kutoka msingi kisha juu yawekwe wavu kuzunguka banda lakini wakati huohuo banda hilo lijengwa kwa kukinga upepo na upande ule wa upana kwa kuta zake zote mbili zinapaswa ziinuliwe tofari hadi juu kabisa ili kukinga upepo lakini vilevile paa lake lipande juu sana ili kupooza hali ya joto linalotokana na jua kali wakati wa mchana.
Banda la kuku linatakiwa liwe na hewa ya kutosha ili liruhusu kuku kupata hewa safi. Mara nyingi kinyesi cha kuku kinatoa harufu kali ya amonia inayotengeneza hewa ya kuchomachoma na hivyo kuleta adha kwa kuku wenyewe na Binaadamu halikadhalika.
Kimsingi Muundo wa banda bora lazima liwe na karido kama inavyooneka katika ramani ya banda hapo chini. Korido hiyo inasaidia kufanya wageni wanapoingia bandani wasiingie moja kwa moja walipo kuku na kuwaletea magonjwa. Lakini, hata hivyo, ndani ya korido, pale mlangoni, unapoingia kuna kijidimbwi cha maji ambacho kinachanganywa na dawa ya kuua wadudu na kila mtu anayeingia ndani humo anapaswa kwanza kukanyaga maji hayo ili kuua wadudu wasababishwa magonjwa kutokana na kutembea huku na kule au daktari wa mifugo anapokuja kwako huku akiwa alitangulia kupita kwenye mabanda mengine ya wafugaji na ikatokea mabanda hayo labda yalikuwa na uambukizo wa magonjwa, itasaidia magonjwa hayo yasiingie kwenye banda lako kwa kuwa atakapokanyaga maji yale ya dawa pale mlangoni wadudu wote watakufa na hivyo kuku wako wakabaki katika mazingira salama kabisa. Wafugaji wengi huweka maji ya dawa ya kuulia wadudu nje ya banda mlangoni matokeo yake huwakiwa na jua na hatimae kupunguza nguvu yake na wakati mwingine kukauka kwa haraka. Maji yaliyochanganywa na dawa ya kuulia wadudu kama yakikaa kivulini yatapaswa kubadirishwa kwa wiki mara moja. Na dawa inayotumika kwa ajili ya kuchanganyia kwenye maji ya kukanyaga mlangoni ni V- RID Disinfectant na au dawa nyingine yoyote inayofanana na hiyo itakayoshauriwa na dakatari wako.
Na kama utahitaji michoro ya mabanda mabalimbali ya kuku tafadhali wasiliana nasi kwa gharama nafuu kabisa. Kinasoru East Africa Tanzania Ltd imedhamiria kukupa elimu itakayokufanya uendeshe mradi wako wa ufugaji kwa kwa kujiamini kabisa kutoka na maarifa tunayokupatia.





MAFANIKIO YANATAKA UTHUBUTU

Kijana huu ni wakati wako. Jaribu kufanya kila jambo linalowezekana katika kutafuta mafanikio. Usitumie njia za panya, tafuta njia halali njia itakayokufikisha kule unakotaka kufika . Katika kutembea au kupita katika njia hiyo, utakutana na vikwazo vingi, usirudi nyuma songa mbele. Kuwa kama mwanajeshi anapokuwa mstari wa mbele vitani, hakuna kurudi nyuma.
Maamuzi yako ni muhimu ukayasimamia mwenyewe. Si kila mtu anapenda ufanikiwe. Yakupasa kuchagua watu au rafiki wazuri wa kukushauri juu ya mipango yako. Lakini pia unaposhauriwa nawe uwe na akili yako binafsi, akili huru iliyotulia inayoweza kuchuja katika yale unayoshauriwa. Ushauri mzuri chukua na ule usiyofaa ukache mara moja.
Elimu ni nyezo ya kukurahisishia kufika kule unakotaka kufika kwa kukuwezesha kuona fursa mbalimbali. Elimu si lazima iwe ile ya darasani, hata ile ya nje ya darasa inafaa ilimrdi tu ikupe mwanga na uweze wa kuona fursa na kujua namna ya kuziendea. Fedha ni kikwazo kwa watu wengi. Ili utimize malengo yako unahitaji kwanza rasilimali fedha. Namna gani utaweza kupata fedha. Benki hazikopeshi watu wasiyokuwa na dhamana. Hakuna taasisi iliyo wazi kwa ajili ya kusaidia wajasiriamali wachanga.
Nini utafanya. Ni muhimu kidogo ulichonacho uweze kuanza nacho hicho hicho hata kama kwa mradi mdogo. Usikidharau. Wahenga walisema ndondondo si chololo. Jifunze kujiwekea akiba kidogokidogo. Usichague kazi. Ulipo tengeneza vikoba kwa kuwashirikisha vijana wenzako wenye kiu ya kufanikiwa. Mara kwa mara jiwekeeni akiba na kisha mkopeshane wenyewe kwa wenyewe. Uaminifu ni kitu cha msingi sana katika kuyafikia malengo yako.
Kama unaujuzi wowote hakikisha unautumia vizuri, unaweza kuwa mkombozi wako. Tufuta kipawa chako. Kitu gani unakiweza kukifanya kwa ufasaha. Jibidiishe kwenye hicho mwishowe utachomoka.
Futa josho lote linalokutiririka usoni kwako, vumilia jua kali linalokupiga mchana kutwa na mwombe sana Manani muumba wa wote akuongoze vyema katika chaguo lako. Mwishowe ili methali isemayo mchumia juani hulia kivulini itatimia kwako. Na hizi siyo ndoto. Kitu cha msingi usikubali kushindwa. Hapa unapaswa kutambua kuwa hata mtoto ili aweze kusimama ni lazima awe amedondoka sana katika harakati zake za kujifunza kusimama na wakati mwingine, katika harakati hizo, atapata michubuko na kuumia lakini haachi kujifunza kusimama.
Hasara katika mradi au biashara haikwepeki. Kuna watakao kudhulumu katika michakato yako mbalimbali ya kujaribu kuusimamisha mradi wako au biashara yako. Haimaanishi kuwa usifanye mradi huo kwa kuogopa kupata hasara. Hasara ni katika changamoto za kujaribu. Ni sehemu ya kujifunza ulipokosea ili badae usirudie makosa yaleyale. Ndiyo maana ukikaa na yeyote aliyefanikiwa akakupitisha katika mapito yake hakika utatoa machozi.
Mafanikio yanataka uthubutu. Lazima kwanza ujitoe akili na ufanye unachokiamini kuwa kitakuvusha. Ziba masikio usisikilize kelele za watu. Endelea kutumbikiza pesa katika mradi wako au biashara yako bila kujali mara ngapi umefeli au utafeli muhimu ni imani uliyonayo katika huo mradi na jitahidi kufuatilia taarifa za mradi wako mara kwa mara ili upate njia bora zaidi za kuuendea mradi huo ili uweze kuwa na tija.

KINASORU EAST AFRICA TANZANIA LTD

KARIBU KWENYE BLOG YETU YA KINASORU EAST AFRICA TANZANIA LTD